Pata Habari Motomoto kwa kuandika E-mail yako hapo chini.


Home » » WANACHUO UALIMU WATIMULIWA BAADA YA KUDUNGWA MIMBA WAKISAKA MAJI...

WANACHUO UALIMU WATIMULIWA BAADA YA KUDUNGWA MIMBA WAKISAKA MAJI...

Imeelezwa kuwa, uhaba wa maji katika Chuo cha Ualimu Murutunguru wilayani Ukerewe, umesababisha athari kadhaa kwa wanachuo, ikiwa ni pamoja na matukio ya ujauzito kwa wanachuo wa kike.

Hayo yalibainika hivi karibuni wakati wa mahafali ya 19 kwa wahitimu wa mafunzo ya ualimu daraja la III A yaliyofanyika chuoni hapo.
Katika risala ya Mkuu wa Chuo hicho kilichoanzishwa miaka 61 iliyopita, Augustine Sahili alisema miongoni mwa wanachuo 14 wa kike waliopaswa kuhitimu mwaka huu, sita walikatisha masomo kutokana na ujauzito.
Alifafanua kuwa, wanachuo hutumia muda mwingi kutafuta maji nje ya chuo, hivyo kujikuta wakiingiza katika majaribu ya kuanzisha mahusiano ya kimapenzi na matokeo yake ni baadhi ya wanachuo wa kike kuishia kupata ujauzito.
Alisisitiza pia kwamba, mbali ya adha wanazopata wanafunzi wa kike, kero ya maji kwa ujumla imekuwa ikichangia kuwavurugia wanachuo utaratibu wa kufuata ratiba za masomo.
Mkuu huyo wa chuo alisema tatizo hilo limedumu kwa miaka mingi, kwani wakati chuo kinaanzishwa mwaka 1952,   kulikuwa na kisima kimoja chenye uwezo wa kuhudumia  watu 70 lakini idadi ya watu kwa sasa imefikia 555, lakini havijapatikana vyanzo vingine vya maji.
Wakati mkuu wa chuo akiyasema hayo, wanachuo kwa upande wao, kupitia risala iliyosomwa na Joel Biganza  wameshauri kuimarishwa kwa miundombinu ya chuo huku wakiitaka Serikali kuangalia upya ufaulu kwa mwalimu kupimwa kwa  somo moja la  utambuzi wa ualimu  linalohusisha saikolojia, tathmini, maandalio na  uchunguzi.
Akizungumzia  somo hilo, mkuu  wa chuo, Sahili  alisema  anayefanya  vibaya katika  somo hilo  anakuwa  ameshindwa  na kuongeza kuwa  mwaka jana wahitimu  watatu  walishindwa  na kurudishwa nyumbani.
Naye Mwakilishi wa  Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Maiga  Joseph  aliutaka uongozi wa chuo hicho kufikisha kilio cha maji kwa mamlaka husika ili iangalie jinsi ya kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.
Katika  mahafali hayo,  walimu 330 walihitimu na kupata cheti cha  ualimu daraja la  III A, idadi ambayo inatarajiwa kuendelea kupunguza kero ya upungufu wa walimu nchini.

 

Copyright © 2009. MCHAMBUZI - Haki zote zimehifadhiwa